Friday, October 21, 2016

Kanda ya Ziwa bila maji: Ukosefu wa maji unavyoathiri elimu


 Mr.Mwalimu Blog

Kero ya maji katika kanda ya Ziwa ni jambo la kustaajabisha sana kwa watu ambao hawajawahikufika ukanda wa ziwa, kwa sababu wao picha walioyonayo kichani ni tofauti na hali halisi. Wengi tunaposema kanda ya ziwa kuna shida ya maji hawaamini lakini ndiyo ukweli.

Mikoa ya Mwanza, Geita, Mara na Simiyu ni moja ya mikoa yenye uhaba mkubwa wa maji licha ya kulizunguka ziwa Victori ambalo lingeweza kuwa chanzo mbadala cha maji. Wakazi wengi wa maeneo haya wanatumia maji yasiyo salama na machafu. Mathalani, Mkoa wa Mara ambao umepitiwa na Ziwa victori una kero kubwa ya maji hata kwa wakazi wanaoishi jirani na ziwa hilo.

Mkoa wa Mara na wilaya zake kama Rorya, Tarime, Bunda, na Serengeti bado hawajanufaika na uwepo wa Ziwa Victoria kama chanzo cha maji. Mkoa huu ambao pia una chanzo kingine kikubwa cha maji kama kingewekewa mikakati mizuri ambacho ni Mto Mara, wakazi wake hawana uhakika wa kupata huduma ya maji!

Inashangaza kama Mufindi ilivyoshangaza kuwa miongoni mwa wilaya ambazo wanafunzi wanakaa chini kutokana na ukosefu wa madawati licha ya kwamba Mufindi ndiyo wilaya inayoongoza kwa kuzalisha miti, mbao na kusambaza kwa nchi nzima! Na kanda ya ziwa ni hivyo maji ya Ziwa victori yamepelekwa mkoa wa Shinyanga, ambako ni mbali sana na ziwa lilipo lakini Geita, Mara, Simiyu ambako ndiko ziwa liliko hakuna maji.

Kama ilivyo mikoa mingine ambayo haina mito wala maziwa, wakazi wa kanda ya ziwa wanasumbuliwa na kero ya maji kama wao. Mathalani Maeneo ya jirani na Shirati, na kata kadhaa za wilaya ya Rorya, Komaswa kwa upande wa Tarime, maji yanauzwa mapaka shilingi mia 400 na 500 kwa lita ishirini. Na maji yanayonunuliwa kwa bei hiyo bado si salama.

Mikoa ya kanda ya ziwa ambayo wakazi wake wengi ni wafugaji, wanategemea maji ya mvua, maji yaliyovunwa kupitia mvua yakiisha, wakazi wa kanda ya ziwa wanatumia maji ya kwenye malambo ambayo pia yanatumika kunyweshea mifugo.

Ukosefu huu wa maji  unaathiri mfumo mzima wa maisha ya wakazi wa kanda ya ziwa kwa sababu bila maji hakuna uhai, hakuna afya bora, hakuna furaha ya maisha. Fikiri baadhi ya maeneo ya mikoa ya kanda ya Ziwa wakazi wake wanatumia zaidi ya saa nne ili kupata maji toka umbali wa kilometa  zaidi ya kumi.
Uhaba wa maji unaathari kubwa sana katika sekta ya elimu, wanafunzi wa mikoa ya kanda ya ziwa wanaumizwa zaidi na hali hii, kwa kweli ni wahanga wa kuu wa kero ya ukosefu wa maji.

Penye ukosefu wa maji safi na salama, hapana afya bora. Magonjwa ya tumbo ni moja ya changamoto kubwa sana kwa afya ya wanafunzi wa kanda ya ziwa. Wanafunzi wengi huugua magonjwa ya tumbo hivyo kushindwa kuhudhuria masomo. Katika siku 192 za masomo kwa mwaka, zaidi ya siku thelathini zinapotea bila kuhudhuria masomo kutokana na kusumbuliwa na magonjwa ya tumbo!

Kero ya maji inasabisha mahangaiko makubwa kwa wanafunzi, hii ni kwa sababu shule nyingi hazina visima wala mabomba ya maji. Katika shule hizi wanafunzi hulazimika kubeba vidumu vya maji kutoka nyumbani ili kumwagilia maua na miti ya mazingira ya shule pia kwa ajili ya huduma ya choo. Wakati mwingine wanafunzi wanatumia muda mrefu kwenda kufuata maji mara baada ya kuripoti shule kiasi wanakosa vipindi vyote vya asubuhi.

Ukosefu wa maji unaathiri pia ratiba ya wanafunzi kujisomea nyumbani mara baada ya kurejea kutoka shule. Ili mwanafunzi afanye vizuri katika masomo lazima apate muda wakutosha kujisomea baada ya saa za shule.

Wanafunzi wengi wa kanda ya ziwa hawana muda wa kujisomea, maana mara tu wanaporejea kutoka shule wanafanya safari nyingine ndefu na yenye mikiki mikiki mingi kwenda kufuata maji. Huko licha ya kusafiri umbali mrefu hukutana pia na foleni kubwa kiasi hupoteza saa nyingi zaidi ambazo wangeweza kuzitumia katika masomo.

Kero hii ya maji inaathiri pia walimu, walimu waliopelekwa na serikali maeneo haya ya kanda ya ziwa, wanakatishwa tamaa pia na hali ya ukosefu wa maji. Gharama kubwa ya kupata maji, muda mwingi unaotumika ili kupata maji vinaathiri ufundishaji wa walimu katika shule zao.

 Wanafunzi wanakosa masomo kwa sababu walimu wanatumia muda mwingi kufuata maji. Hali hii pamoja na maji yenyewe kuwa si masafi na salama imechangia walimu wengi kutopendelea kufanya kazi katika vijiji ambavyo vinashida ya maji. Baadhi wamelazimika kuhama haraka au hata kuacha kazi.

Usafi binafsi wa wanafunzi kama vile kuoga, kufua na kadhalika vinakuwa vigumu kwa wanafunzi kwa sababu ya ukosefu wa maji. Mwanafunzi anatakiwa pia kujifunza kujiweka nadhifu, ufundishaji unadhifu kwa vitendo kwa vijana wetu unakuwa mgumu kwa sababu ya shida ya maji. Kuna wakati mwanafunzi anavaa ngua chafu inabidi tu mwalimu uvunge maana unajua kinachomsibu.

Ushauri wangu kwa viongozi wa mikoa ya kanda ya Ziwa na wilaya zake, wakuu wa halmashauri na madiwani, wabunge wote bila kujali wajimbo ama wa kuteuliwa suala la ukosefu wa maji liwe ajenda kuu katika vikao na litekelezwe kwa vitendo.Ni aibu na uzembe kanda ya ziwa kukosa maji.\

Pia wananchi wa kanda ya ziwa ni wakati wakudai maji bila kusita bila uitikadi wa vyama, katika kila kikao tunachokaa na viongozi wetu tuwaambie MAJI KWANZA.MR.MWALIMU.BLOGSPOT.COM, ELIMU KWANZA.

Share this

0 Comment to "Kanda ya Ziwa bila maji: Ukosefu wa maji unavyoathiri elimu"

Post a Comment

New post Overview  Posts Pages Comments Stats Earnings Campaigns Layout Template Settings 1401 1409

Post a Comment

1410

1411 1412 1413 1414

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...